Saturday, January 3, 2015

Taarifa ya Tume ya Uchaguzi kuhusu Zoezi la BVR la Kuboresha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura

Mfano wa mashine ya mfumo wa BVR
Ndugu Waandishi wa Habari, Mkurugenzi wa Uchaguzi, Watendaji wa Tume, Mabibi na Mabwana.
Kwa niaba ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi, napenda kuchukua fursa hii kuwakaribisheni kwa mara nyingine katika Mkutano huu. Nawashukuru kwamba, pamoja na majukumu mengi mliyo nayo, mmeweza kuupa umuhimu wa pekee mkutano wetu huu na kuhudhuria kwa wingi. Kwa niaba ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi, nasema Ahsanteni na Karibuni sana.


Katika mkutano huu, Tume inalenga kutoa taarifa kuhusu tathmini ya utekelezaji wa zoezi la majaribio ya Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura (Pilot Registration) kwa mfumo wa Biometric Voters Registration (BVR) zoezi ambalo lilikamilika wiki iliyopita.
Ndugu Wanahabari, Tume ya Taifa ya Uchaguzi, imepewa jukumu la kisheria Kuandikisha Wapiga Kura katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuliboresha Daftari hilo kwa ajili ya Uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wabunge na Madiwani. Kwa mujibu wa Sheria ya Kura ya Maoni, Daftari hili la Kudumu pia litatumika katika Kura ya Maoni kuhusu Katiba Inayopendekezwa.

Ndugu Wanahabari; mtakumbuka kuwa, Tume ya Taifa ya Uchaguzi imekuwa katika mchakato wa Maandalizi ya Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa kutumia Teknolojia Mpya ya ”Biometric Voter Registration” (BVR) na mara kwa mara imekuwa ikiomba kukutana nanyi ili kuwapa taarifa kuhusu hatua mbalimbali ambazo Tume imekuwa ikizipitia.

Kwa kuwa Uboreshaji huu ulihusisha matumizi ya vifaa vya teknolojia ya kisasa, vifaa ambavyo vilikuwa havijawahi kutumika katika Uboreshaji nchini, tuliona si vyema kuagiza vifaa vingi kabla ya kuvifanyia majaribio. Zoezi la majaribio lilifanyika ili kuwa na uhakika kuwa vifaa hivi vya Biometric Registration vina uwezo wa kuandikisha Wapiga Kura katika mazingira ya nchi yetu.

Zoezi hili liliangalia uwezo wa watendaji kutumia BVR katika uandikishaji na pia uwezo wa vyombo vyenyewe katika Software na Hardware kwenye uandikishaji. Katika zoezi hili tuliangalia changamoto zilizojitokeza ili kuzipatia ufumbuzi kabla ya kuanza Zoezi halisi la Uandikishaji wa nchi nzima.

Ndugu Wanahabari, Kama nilivyosema, Tume inakutana nanyi ili kuwapa taarifa kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa zoezi la Majaribio la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililofanyika kwa siku saba (7) katika Kata za Bunju na Mbweni katika Jimbo la Kawe, Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es salaam; Kata za Ifakara, Kakingiuka, Ipangala, Mlabani na Viwanja Sitini katika Jimbo la Kilombero Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero, mkoani Morogoro; na Kata za Ikuba, Usevya na Kibaoni katika Jimbo la Katavi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele mkoani Katavi.
Tume kwa namna ya pekee, inawashukuru sana Waandishi wa Habari kwa kujitokeza na kufuatilia zoezi hili la majaribio ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura. Waandishi wa Habari wamesaidia sana katika kuhamasisha Wananchi wa Majimbo husika kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura. Vilevile, Waandishi wa Habari wamesidia katika kutoa taarifa za maendeleo ya zoezi hili kitu ambacho kimesaidia kufanikisha zoezi hili.
Jumla ya BVR Kits 250 zilitumika katika Uboreshaji huo kwa mgawanyo ufuatao:- Halmashauri ya Kilombero BVR Kits 80, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele BVR Kits 80 na Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni BVR Kits 90. Vituo katika Kata zote vilikuwa vinafunguliwa saa 2.00 asubuhi na kufungwa saa 12.00 jioni.
Ndugu Waandishi wa Habari, Tume inapenda kuwafahamisha kuwa zoezi hilo la Majaribio ya Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura katika majimbo matatu yaliyotajwa limefanyika na kukamilika kwa mafanikio makubwa. Changamoto zilizojitokeza hapa na pale zimetusaidia kupata ufumbuzi ambao utatusaidia wakati wa Uandikishaji wenyewe nchi nzima. Tunasema mafanikio makubwa kwa sababu matokeo ya jumla yanaonyesha kuwa idadi ya wapiga kura waliojitokeza kujiandikisha ilikuwa kubwa na kuvuka malengo ya waliokadiriwa kuandikishwa.

Mkoa wa Dar es salaam, Kata za Bunju Wapiga Kura 15,123 waliandikishwa kati ya 27,148 na Kata ya Mbweni Wapiga Kura 6,200 waliandikishwa kati ya 8,278. Takwimu hizi za waliondikishwa inatokana na makisio ya watu tuliyokuwa tumejiwekea kutokana na matokeo ya sensa mwaka 2012. Mkoa wa Morogoro Kata za Ifakara, Kakingiuka, Ipangala, Mlabani na Viwanja Sitini Wapiga Kura walioandikishwa ni 19,188 wakati makisio yalikuwa watu 17,790 na Mkoa wa Katavi Halmashauri ya Mlele kata za Ikuba, Usevya na Kibaoni Wapiga Kura 11,210 waliandikishwa wakati makisio yalikuwa watu 11,394. Matokeo haya yanadhihirisha kuwa vifaa vya uandikishaji vilifanya kazi vizuri na hivyo vinaweza kutumika katika Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa nchi nzima.

Pamoja na mafanikio hayo, kama ilivyo kawaida katika majaribio yoyote kwani ndiyo lengo la kufanya majaribio, zilikuwepo changamoto kadhaa wakati wa utekelezaji wa zoezi hilo. Changamoto hizo zinaweza kuwekwa katika makundi makubwa matano kama ifuatavyo:- 

i. Matatizo yaliyotokana na ’Settings’ za BVR Kits; 
  • Baadhi ya ”BVR Kits” zilitumia camera iliyo katika Laptop badala ya camera iliyowekwa kwa ajili ya kupiga picha. 
  • Uchukuaji wa alama za vidole (Automatic Process settings) ilisababisha Mfumo kusimama (Crash). 
  • Tatizo la kuchukua picha iwapo viwango vya ICAO vya ubora wa Picha havijafikiwa kama 
  • Unrecognise face, 
  • Unrecognise eye, 
  • Stretch photo, 
  • Un even light. 
  • Uwepo wa Majina yenye ”apostrophe”. 

ii. Matatizo yaliyosababishwa na Software; 
  • Fingeprint Scanner kusababisha Mfumo wa Uandikishaji kusimama (Crash) kutokana na SDK na za vifaa finger print scanner. 
  • Kuharibika kwa baadhi ya file (File Corruption) kutokana na d11 ya finger print scanner. 

iii. Matatizo ya hardware; 
  • Komputa (Laptop) Kupata Joto kutokana na Bati liliwekwa kuzuia kuibiwa Laptop kwa urahisi ambapo mahitaji kuwezesha mzunguko wa hewa ndani ya ”BVR Kit”. 
  • FlashDrive ya pili (Drive G) kutoonekana hivyo kuhitaji kubadilishwa na kuwa SD card. 
  • Uharaka wa uchukuaji alama za vidole ambapo ilibidi kufanya mabadiliko. iv. Matatizo ya lojistiki na matatizo ya Watendaji wa zoezi la Uandikishaji. 
  • ”BVR Kit” kuchelewa kufikishwa katika Vituo. 
  • Vurugu wakati wa uandikishaji ambao unahitaji Ulinzi kuwepo. 
  • Baadhi ya ”BVR Operator” kutokuwa na uwezo au kuwa makini katika utumiaji wa ”BVR Kits” hivyo kuhitaji elimu zaidi kwa ”BVR Kit Operator”. 
  • ”BVR Kit Operator” kubadili Kits kwa tatizo dogo linaloweza kutatulika kwa urahisi. 
  • ”BVR Kit Operators” kutokuwa na uelewa wa matumizi ya ”Solar Panel” kwani baadhi ziliwekwa chini ya mti au kutogeuzwa kadri muda ulivyokuwa unakwenda. 

Mbali ya changamoto hizo zilikuwepo pia changamoto nyingine za kimiundombinu na kibinadamu. Miongoni mwa changamoto hizo ni pamoja na Hali ya Hewa hususan katika jiji la Dar es salaam na Morogoro. Mtakubaliana nami kuwa pamoja na kuwa jiji la Dar es salaam kwa kawaida lina hali ya hewa ya joto lakini kwa takribani mwezi mmoja hivi uliopita kumekuwa na ongezeko la joto hali iliyosababisha hata baadhi ya vifaa vya kuandikishia hususan ’BVR Kits’ wakati mwingine kushindwa kufanya kazi inavyotakiwa na hivyo kusababisha shughuli za uchapishaji wa Kadi za Kupigia Kura kuchelewa.

Aidha, ushirikiano mdogo kutoka kwa Wananchi nao ulikuwa changamoto iliyosababisha zoezi hilo kwenda taratibu. Baadhi ya wananchi kushindwa kuzingatia maelekezo yaliyokuwa yakitolewa na BVR Kit Operators kutokana na uelewa duni kwani ilibainika pia kuwa bado kuna idadi kubwa ya wasiojua Kusoma na Kuandika. Hali hiyo ilifanya zoezi la Uchukuaji wa alama za Vidole (Fingerprint) na Utiaji wa Saini kuwa mgumu.

Kadhalika kumekuwepo na mwamko mkubwa kwa wananchi kujitokeza kwa wingi ili kujiandikisha. Hivyo, kulikuwepo na watu wengi sana katika vituo vya Uboreshaji wa Daftari hilo la Kudumu la Wapiga Kura. Changamoto zote zilizojitokeza kuhusiana na settings tuliweza kwa ushirikiano na watengenezaji wa vifaa hivyo, kuzipatia suluhisho wakati zoezi linaendelea. Pia chanagamoto za ’software’ nazo zimekwishapatiwa suluhisho.

Changamoto kuhusu hardware zitarekebishwa wakati wa utengenezaji wa BVR Kits 7,750 ambazo zilikuwa hazijaanza kutengenezwa kusubiri matokeo ya zoezi hili la majaribio.Marekebisho hayo ya hardware pia yatafanywa katika BVR Kits 250 zilizoletwa kwa ajili ya majaribio. Changamoto kuhusu fedha na lojistiki zinaendelea kushughulikiwa kwa ushirikiano na Serikali. Kuhusu changamoto za Watendaji tunaendelea kuzishughulikia kwa kuhakikisha Watendaji tutakaowatumia wanakuwa na utaalam unaotakiwa kuziendesha BVR Kits hizo.

Ndugu Waandishi wa Habari, Napenda pia niongelee baadhi ya masuala yanayohusu zoezi la Uboreshaji wa Majaribio kwa ujumla. Kwanza ni vyema ieleweke wazi kuwa kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 na kwa ajili ya Kura ya Maoni ya Katiba Mpya, Mpiga Kura atatumia Kitambulisho cha Mpiga Kura alichopatiwa na Tume baada ya kuandikishwa katika mfumo huu tu na si vinginevyo. Vitambulisho vilivyotolewa katika uboreshaji huu wa majaribio ni vitambulisho halisi hivyo kila aliyejiandikisha katika zoezi hili la majaribio ni muhimu atunze kadi yake kwa ajili ya matumizi yaliyotajwa kwa kuwa taarifa zake tayari zimeingia katika Kanzi data ya Tume hivyo hataweza tena kujiandikisha kwa mara nyingine hata kama atabadilisha kituo cha kujiandikishia.

Ndugu Wanahabari, Pili, ni muhimu wananchi wakapata taarifa hizi kwa usahihi kwa vile wapo baadhi ya Watu wanaodhani kuwa kwa kuwa hilo lilikuwa ni zoezi la majaribio basi watakuwa na fursa nyingine ya kujiandikisha wakati wa zoezi la nchi nzima. Napenda nisisitize hapa kuwa kwa yeyote aliyejiandikisha katika zoezi hili, hatatakiwa tena kujiandikisha labda tu kwa yule ambaye atahitaji kubadilisha taarifa zake kutokana na sababu kama zilivyofafanuliwa na Tume.

Ndugu Wanahabari. Napenda nisisitize pia kuwa, Tume ya Taifa ya Uchaguzi inayo dhamira ya dhati ya kukuza demokrasia kwa kuandaa na kuendesha chaguzi zake katika mazingira rafiki na wazi yatakayotoa fursa kwa kila raia wa Tanzania aliyetimiza umri wa miaka 18 kutumia haki yake ya kikatiba ya kuchagua viongozi wake. Tume itakuwa tayari kupokea maoni na ushauri kutoka kwa wadau mbalimbali wa Uchaguzi kuhusu namna bora ya kufanikisha majukumu yake. Aidha, Tume itaendelea kubuni mbinu na mikakati itakayoboresha utendaji kazi wake.

Ndugu Waandishi wa Habari,
Kwa kumalizia, ninapenda tena kuwashukuru wote kwa kuhudhuria Mkutano huu. Tume mara zote imekuwa ikitambua mchango wa Vyombo vya Habari katika kufikisha ujumbe kwa jamii inayokusudiwa. Hali kadhalika, katika zoezi hili la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa kutumia BVR vyombo vya habari vimekuwa mstari wa mbele katika kuufahamisha umma wa watanzania na kuhamasisha wale wote wenye sifa kujitokeza na kujiandikisha. Tume inatambua na kuthamini mchango wenu huo.

Kwa mantiki hiyo, na kwa mara nyingine natoa rai kwenu na Wadau wengine wa Uchaguzi kutoa taarifa zilizo sahihi na kuhamasisha Wananchi kushiriki katika zoezi hilo kubwa linalotarajia kuanza wakati wowote kuanzia sasa. Ni mategemeo ya Tume kuwa kwa kupitia kalamu na vipaza sauti vyenu taarifa hizi zitawafikia Wapiga Kura wetu na hatimaye wataweza kujitokeza kwa wingi na kujiandikisha pindi muda huo utakapowadia.

Ndugu Wanahabari,
Nimalizie pale nilikoanzia, kwamba uandikishaji wa majaribio katika baadhi ya Kata za Majimbo matatu ya Kawe, Kilombero na Katavi umefanikiwa kwa kiwango kikubwa licha ya changamoto zilizojitokeza. Kutokana na changamoto hizo, vifaa vya BVR vitakavyo tumika katika zoezi la Kuboresha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura nchini kote vitafanyiwa marekebisho stahili kwa vile 7,750 ambavyo bado havijafika nchini, pamoja na vile 250 vilivyotumika katika zoezi la majaribio.

Hivyo, hapana shaka kwamba, kama mambo yote yataendelea kama ilivyopangwa hadi sasa, mpango wa kuendesha Kura ya Maoni mwishoni mwa Aprili 2015, na Uchaguzi Mkuu October, 2015 kwa kutumia Dafti lililoboreshwa na vifaa vya BVR uko pale pale. Kama kawaida, ili kufanikisha ratiba hiyo, ushirikiano wa kila Mdau -Vyama vya Siasa, Vyama visivyo vya Kiserikali NGO’s, CSO’s, Serikali, Wananchi wote, Wapiga Kura na Wafadhili wote, Tume inaomba uendelee kwa kiwango cha juu. Hili likifanyika, Tume inaamini kuwa zoezi la Kura ya Maoni na Uchaguzi Mkuu Octoba, 2015 utafanikiwa kwa amani na utulivu. Hayati Mwalimu J. K. Nyerere alisema, Inawezekana, Timiza Wajibu Wako.

Mwisho kabisa lakini muhimu sana, kwa niaba ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi naomba kwa msisitizo kwamba zoezi likianza, wanachi nchini kote wajitokeze kwa wingi kujiandikisha. Hii itawawezesha kwanza kupiga Kura ya Maoni na baadaye katika Uchaguzi Mkuu, Octoba, 2015. Kukosa kufanya hivyo ni kujinyima HAKI YAKO YA KIKATIBA YA KUCHAGUA VIONGOZI MNAOWATAKA

8 comments:

Unknown said...

It is amazing, I wish I wuld have mine like this.How did you make it

Unknown said...

I hope technology is helping and supporting all things like this, I really like it.

Unknown said...

how did you attachech link and picture on a page.
SWALEHE Fakii said

Unknown said...
This comment has been removed by the author.
Unknown said...
This comment has been removed by the author.
Unknown said...

Technology is very essence in trying moving our country to some place better,but we do not have have to take charge in any any technological that fast,slow moving brings have advantage to something helped for future useful,i do not thing if the thing is trustful to Tanzanian people.#DIT- Kalula Alex E

Unknown said...

I like it.
#DIT, Matambala Modestus F.

Unknown said...

Huu mfumo wanaotaka kutumia una matatizo mengi.#DIT